Release No.
066
TAARIFA KWA VYOMBO VYA
HABARI
Mei 1, 2012
NGORONGORO HEROES KWENDA
SUDAN MEI 2
Timu ya Taifa ya vijana wenye
umri chini ya miaka 20 (Ngorongoro Heroes) inatarajia kuondoka kesho (Mei 2
mwaka huu) kwenda Sudan kwa ajili ya mechi dhidi ya Sudan itakayochezwa Mei 5
mwaka huu.
Msafara wa Ngorongoro Heroes
utakaokuwa na watu 28 ukiongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Athuman Kambi utaondoka saa 8.45 mchana kwa
ndege ya Kenya Airways.
Ngorongoro Heroes itaagwa
rasmi kwa kukabidhiwa Bendera ya Taifa kesho (Mei 2 mwaka huu) saa 5 kamili
asubuhi kwenye ofisi za TFF zilizoko Uwanja wa Kumbukumbu ya
Karume.
Wengine katika msafara huo ni
wachezaji na benchi la ufundi linaloongozwa na kocha Kim Poulsen. Mechi hiyo ya
marudiano namba 16 itachezwa kwenye Uwanja wa Khartoum kuanzia saa 2 kamili
usiku kwa saa za Sudan.
Iwapo Ngorongoro Heroes
ambayo ilishinda mechi ya kwanza mabao 3-1 itafanikiwa kuitoa Sudan itacheza na
Nigeria ambayo yenyewe imefuzu moja kwa moja kucheza raundi ya pili ya michuano
hiyo.
Mechi ya kwanza itachezwa
Julai 28 jijini Dar es Salaam wakati ya marudiano itafanyika Nigeria kati ya
Agosti 10, 11 na 12 mwaka huu. Fainali za U20 kwa Afrika zitafanyika Machi
mwakani nchini Algeria.
MECHI KUCHANGIA TWIGA STARS
SASA MEI 6
Mechi maalumu ya hisani kwa
ajili ya kuchangia timu ya Taifa ya wanawake (Twiga Stars), kati ya timu hiyo na
wasanii wa filamu maarufu kama Bongo Movie itachezwa sasa itachezwa Mei 6 mwaka
huu badala ya Mei 4 mwaka huu.
Kwa mujibu wa kampuni ya Edge
Entertainment iliyoandaa mechi hiyo, imesogezwa mbele kwa siku mbili kutoa fursa
kwa watu wengi zaidi kujitokeza kuchangia Twiga Stars. Awali ilikuwa ichezwe
Ijumaa ambayo ni siku ya kazi, hivyo imesogezwa hadi Jumapili ambayo ni siku ya
mapumziko.
Mechi hiyo itachezwa Uwanja
wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni ambapo viingilio kwa viti vya rangi
ya chungwa, kijani na bluu ni sh. 2,000, VIP C na B itakuwa sh. 5,000 wakati VIP
A ni sh. 10,000.
Twiga Stars ambayo kwa sasa
haina mdhamini na kambini katika kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ya Ruvu
mkoani Pwani kujiandaa kwa mechi ya mashindano ya Afrika kwa Wanawake (AWC)
dhidi ya Ethiopia.
Timu hizo zitapambana Mei 26
mwaka huu jijini Addis Ababa na kurudiana Juni 16 mwaka huu Uwanja
wa Taifa, Dar es Salaam. Mshindi atashiriki fainali za AWC zitakazofanyika
Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea.
RUFANI YA AFRICAN LYON
KUJADILIWA MEI 2
Kamati ya Nidhamu ya
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inatarajia kukutana Mei 2 mwaka huu
kujadili rufani iliyowasilishwa mbele yake na klabu ya African
Lyon.
Klabu hiyo ya Ligi Kuu
inailalamikia TFF ikipinga uamuzi uliofanywa na Kamati yake ya Ligi juu ya
kuvunjika kwa pambano la ligi hiyo kati ya Azam na Mtibwa Sugar lililochezwa
hivi karibuni kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
Katika rufani yake, Lyon
imedai uamuzi uliofanywa na Kamati ya Ligi ya TFF haikuwa sahihi, kwani
haukuzingatia kanuni za ligi hiyo kuhusu timu inayogomea mchezo.
Kamati hiyo chini ya Kamishna
Mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana inatarajia kufanya kikao chake kuanzia 8
mchana.
PONGEZI KWA TIMU YA
SIMBA
Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa timu ya Simba kwa ushindi wa mabao 3-0 ambao
iliupata juzi (Aprili 29 mwaka huu) dhidi ya Al Ahly Shandy ya Sudan katika
mechi ya Kombe la Shirikisho iliyochezwa Dar es Salaam.
Ushindi huo umetokana na
ushirikiano uliopo kuanzia kwa wachezaji, benchi la ufundi, viongozi, wanachama
wa klabu hiyo na Watanzania kwa ujumla.
Ni imani ya TFF kuwa Simba
haijabweteka kwa ushindi huo na badala yake sasa inajipanga kwa ajili ya mechi
ya marudiano itakayochezwa nchini Sudan ili kuondoa Al Ahly Shandy kwenye
michuano hiyo na kusonga mbele.
TFF kama kawaida itaendelea
kutoa ushirikiano kwa Simba ili kuhakikisha inafika mbali kwenye mashindano
hayo, na ikiwezekana kuandikika historia ya kuwa timu ya kwanza ya Tanzania
kutwaa Kombe la Shirikisho.
PAZIA LIGI KUU VPL KUFUNGWA
MEI 5
Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa
2011/2012 kuwania ubingwa wa Tanzania Bara itafikia tamati Mei 5 mwaka huu kwa
bingwa kujulikana ambapo timu zote 14 siku hiyo zitakuwa uwanjani.
Klabu kongwe za mpira wa
miguu nchini Simba na Yanga zitakutanisha timu zao katika mechi itakayochezwa
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Nayo Oljoro JKT itakuwa mwenyeji wa Polisi
Dodoma katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha na
Ruvu Shooting itacheza na Villa Squad katika Mabatini, Mlandizi.
Mechi nyingine zitakuwa kati
ya Coastal Union na Toto African itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini
Tanga, African Lyon na JKT Ruvu (Uwanja wa Manungu, Morogoro), Azam na Kagera
Sugar (Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam) na Moro United na Mtibwa Sugar (Uwanja
wa Jamhuri, Morogoro).
Kwa mujibu wa kanuni namba
4(2)(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom, timu tatu za mwisho katika msimamo wa ligi
zitashuka daraja. Tayari Moro United na Polisi Dodoma zimeshashuka, iliyobaki
itajulikana baada ya mechi za Jumamosi ambazo zote zitaanza saa 10 kamili
jioni.
MIKOA SITA YAOMBA UENYEJI
LIGI YA TAIFA
Mikoa sita imeshaomba kuwa
wenyeji wa Ligi ya Taifa itakayochezwa katika vituo vitatu tofauti. Ligi hiyo
inayoshirikisha mabingwa wa mikoa inatarajia kuanza baadaye mwezi
huu.
Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira
wa Miguu Tanzania (TFF) inatarajia kukutana wakati wowote kupitia maombi hayo
kabla ya kufanya uamuzi wa vituo na tarehe ya kuanza ligi hiyo.
Mikoa iliyoomba vituo ni Dar
es Salaam, Kigoma, Lindi, Mara, Shinyanga na Singida.
Boniface
Wambura
Ofisa
Habari
Shirikisho la
Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Comments