MGOMBEA BINAFSI HATOEPUKIKA 2015

WajumbewaHalmashauriKuuya Chama cha Mapindunzi (CCM), ShamsaMwangunga(kushoto) na Aisha Kigoda, wakitetajambowakatiwaseminayawajumbewahalmashauriKuuyaTaifaya Chama hichomjini Dodoma jana.Pichana Fidelis Felix




Waandishi wetu
SHINIKIZO la wananchi kutaka mgombea binafsi, limeanza kukilainisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuwataka wanachama wake kujiandaa kisaikolojia kwa kukabaliana na wagombea hao katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.

Kwa muda mrefu kumekuwa na shinikizo kutoka kwa watu wa kada mbalimbali, wakiwemo wanaharakati na wanasheria wanaotaka kuwepo kwa mgombea binafsi jambo ambalo pia kiliwahi kupigiwa debe na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere mnamo mwaka 1995.

Mwalimu aliwahi kusema: “Mimi nadhani sheria imekosea kuzuia wagombea binafsi. Hili jambo limekosewa ni la msingi. Ndiyo maana napenda kulisema ni la msingi, linahusu haki yangu na yako ya kupiga kura na kupigiwa kura. Hii ni haki ya uraia.”

Jana, katika kikao cha semina ya viongozi ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM, Kamati iliyoundwa na chama hicho kuangalia jinsi kinavyoweza kuwasilisha maoni yake katika Tume ya Katiba, ilitaka wanachama kujiandaa kwa suala hilo.

Suala la mgombea binafsi limekuwa likipingwa na chama hicho kwa muda mrefu kwa hofu kuwa lingeweza kukiumiza pindi wanachama wake wanaposhindwa kura za maoni, kwani wangeweza kusimama binafsi na kushinda.

Lakini, kamati hiyo ambayo iliongozwa na Mjumbe wa Kamati Kuu (CC), Abdulrahman Kinana, jana ilitoa mapendekezo mbalimbali ikiwamo muundo wa Muungano huku ikiwataka wanaCCM kujiandaa kukabiliana na mgombea huyo binafsi.

Chanzo chetu ndani ya kikao hicho, kilisema miongoni mwa mapendekezo hayo ni Serikali tatu; Shirikisho, Tanganyika na Zanzibar. Pia, kuna pendekezo la Serikali mbili, huku ikitoa manufaa na athari za kila pendekezo.

Mapendekezo mengine ni pamoja na muundo wa Bunge na upatikanaji wa wabunge, ikipendekeza kuwapo kwa mabunge mawili, mojawapo lenye mamlaka ya juu na jingine likiwa na mamlaka ya chini.

Mapendekezo hayo ambayo yataanza kujadiliwa na wajumbe wa Nec, yanaonekana kuwa mtego kutokana na hali ndani ya chama hicho ilivyo hivi sasa.

“Hii inaonekana tumepewa kamba tujimalize wenyewe, maana suala la mgombea binafsi kwa vyovyote vile lazima litakuwa kwenye Katiba Mpya, njia ambazo tumekuwa tukitumia zimefikia mwisho, utashi wa wananchi utachukua mkondo wake, hivyo lazima tujipange,” kilidokeza chanzo chetu.

Katika kikao cha CC juzi, baadhi ya wajumbe walitaka Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa asilaumiwe kutokana na wanachama wa chama hicho kukimbilia Chadema, pia wakipinga George Mkuchika kubaki katika Baraza la Mawaziri.

Moto wa mgombea binafsi

Moto wa kuwepo kwa mgombea binafsi katika chaguzi za kisiasa ulianzishwa na Mchungaji Christopher Mtikila alipofungua kesi ya kikatiba katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma mwaka 1993 akiiomba iruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi.

Katika hukumu iliyotolewa Oktoba 24, 1994 na Jaji Kahwa Rugakingira, Mchungaji Mtikila aliibuka mshindi.

Hata hivyo, Serikali ilikata rufaa Mahakama ya Rufani, lakini wakati rufaa hiyo ikisubiri usikilizwaji na uamuzi, Serikali ilipeleka muswada bungeni na kufanya marekebisho ya kikatiba na kuweka ibara inayotamka kuwa kila mgombea ni lazima awe amependekezwa na chama cha siasa.

Februari 17, 2005, Mchungaji Mtikila alifungua kesi nyingine Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam akipinga marekebisho hayo ya Katiba ya mwaka 1994. Katika kesi hiyo alikuwa akiiomba Mahakama hiyo pamoja na mambo mengine, iamuru kuwepo kwa mgombe binafsi.

Katika hukumu iliyotolewa Mei 5,2006, Mchungaji Mtikila aliibuka mshindi kwa mara nyingine baada ya Mahakama Kuu kukubaliana na hoja na maombi yake na kuwepo kwa mgombea binafsi.

Hukumu hiyo ilitolewa na na jopo la Majaji watatu wa Mahakama Kuu wakiongozwa na aliyekuwa Jaji Kiongozi, Amir Manento, Salum Massati na Thomas Mihayo.

Serikali ilikata tena rufaa katika Mahakama ya Rufani, ikipinga uamuzi huo wa Mahakama Kuu, iliyosikilizwa na Jopo la Majaji Saba wa Mahakama ya Rufani Aprili 8, 2010.

Katika hukumu yake ya Juni 16, 2010, Mahakama ya Rufani ya Tanzania ilitolewa na jopo la majaji hao saba walioongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Augustino Ramadhani, mahakama hiyo ilijifunga mikono baada ya kusema kuwa haina mamlaka ya kutengua ibara ya Katiba.

Wengine katika jopo hilo la majaji walikuwa Eusebio Munuo, Januari Msofe, Benard Luanda, Mbarouk Mbarouk, Nathalia Kimaro na Sauda Mjasiri

Malisa hajafukuzwa
Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Kaimu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana (UVCCM), Benno Malisa, jana walilazimika kutoka nje ya ukumbi wa mikutano na kukutana na waandishi wa habari kukanusha taarifa za kiongozi huyo wa juu wa umoja wa vijana kufukuzwa Kamati Kuu (CC).

Taarifa zilizosambaa juzi na jana, zilidai kuwa Malisa alifukuzwa CC baada ya kuhoji uteuzi wa wakuu wa wilaya ambao Rais Jakaya Kikwete aliufanya hivi karibuni.

Nape alisema hakuna kitu cha aina hiyo na kwamba, hicho ni kati ya vikao vya chama hicho vilivyowahi kufana na kufanyika kwa furaha tofauti na taarifa zilizokuwa zinasambazwa.

Naye Malisa alisema ameshangazwa na taarifa hizo kwa sababu bado ni Mjumbe wa CC na alikuwa akihudhuria kikoa cha Halmashauri Kuu.

Uteuzi Makatibu wa wilaya

Kamati Kuu (CC) ya CCM imefanya uteuzi wa makatibu wa wilaya 32 kujaza nafasi zilizokuwa wazi kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo baadhi kuteuliwa kuwa wakuu wa wilaya na kwamba watapangiwa kazi baadaye.

Makatibu hao ni Grayson Mwengu, Abdallah Hassan, Ernest Makunga, Mgeni Haji, Innocent Nanzabar, Nicholaus Malema, Mercy Mollel, Michael Bundala, Elisante Kimaro, Zacharia Mwansasu, Eliud Semauye, Habas Mwijuki, Loth Ole Nasele na Charles Sangura.

Wengine ni Donald Magessa, Fredrick Sabuni, Janeth Mashele, Daniel Parokwa, Zongo Lobe Zongo, Mwanamvua Killo, Joyce Mmasi, Simon Yaawo, Epimack Makuya, Amina Kinyongoto, Asia Mohammed, Venosa Mjema, Augustine Minja, Elly Minja, Ernest Machunga, Seleman Majilanga, Christina Gukwi na Joel Mwakila.


Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA